Kauli hiyo ya Dk. Mwakyembe imekuja siku chache baada ya kusambazwa kwa
waraka unaodaiwa kuandikwa naye, ukimuhusisha na tuhuma za kumshambulia
Lowassa, jambo ambalo amelifananisha kuwa ni sawa na siasa za kitoto.
Akizungumza jana katika kipindi cha Power Breakfast kinachorushwa na
kituo cha redio Clouds FM, alisema kutokana na kusambazwa kwa waraka
ambao umeandikwa nyadhifa zake za ubunge na uwaziri, hivi sasa
ameshaanza kuchukua hatua za kisheria dhidi ya watu waliokuwa
wakiusambaza.
Waziri Mwakyembe ambaye kitaaluma ni mwanasheria na mwanahabari, alisema
anapata shaka hata na baadhi ya vyombo vya habari pamoja na mitandao
hiyo na kudai kuwa anamshambulia Lowassa.
“Ninashangazwa sana na hii mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya
habari (magazeti), vimekuwa vikiandika vitu vibaya ikiwa ni pamoja na
kumshambulia Lowassa wakati hata siku moja sijazungumza nao.
Dk. Mwakyembe alisema vyombo hivyo vimeshaanza uchunguzi mkali ili kuwabaini watu walioandika na kutuma taarifa hizo.
Dk. Mwakyembe alisema anashangazwa na watu kutumia jina lake kumchafua
kwa kuwa hana tatizo na mtu yeyote na kama chanzo ni suala la Richmond,
ilikuwa ni kazi aliyopewa na Bunge.
Alisisitiza kuwa alifanya kazi hiyo vizuri kwa kumuweka Mungu mbele, lakini si kuongea uongo jambo ambalo si utamaduni wake.
Ofisa Habari wa EU, Susanne Mbise jana alikanusha taarifa izo na
kusema kuwa hata wao wamesikia taarifa hizo, lakini ukweli wa jambo
hilo upo kwenye taarifa waliyoweka kwenye mtandao wa Face Book ya Umoja
huo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyosainiwa na Ofisa anayeshughulikia Siasa
na Habari, Luana Reale wa kitengo cha habari, Balozi huyo hajafanya
mkutano wowote na mwandishi yeyote na kwa maana hiyo hajatoa taarifa
yoyote kwa vyombo vya habari.
Reale alisema kuwa tangu Juni mosi mwaka huu Balozi huyo hayuko nchini
kwani alisafiri kwenda makao makuu ya Umoja huo na hajarejea nchini.
Alisema kuwa EU ina uhusiano mzuri wa muda mrefu na Tanzania ambao umejengwa juu ya misingi ya kuheshimiana na kuaminiana.
EU inatoa taarifa hizo baada ya watu wasiojulikana kusambaza taarifa za
uzushi na uongo kwenye mitando ya kijamii wakidai kuwa Rais Kikwete
ameonywa kwamba Lowassa akipitishwa kuwania urais uhusiano wa Tanzania
na EU utaingia shakani na kwamba hawataisaidia katika miradi ya
maendeleo.
Wazushi hao walidai kuwa Lowassa ni mtuhumiwa namba moja wa rushwa
nchini na kutaja kuwa anahusika katika kadhia ya Richmond na NIC.