Mkuu wa Wilaya ya Geita, Josephat Maganga, amewataka wachimbaji na wachenjuaji wa dhahabu mkoani Geita kuzingatia taratibu na matumizi salama ya kemikali na watakaokwenda kinyume watachukuliwa hatua za kisheria.
Mkuu wa Wilaya ameyasema hayo leo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Geita wakati akifunga mafunzo ya matumizi salama ya kemikali kwa wachimbaji na wachenjuaji wa dhahabu katika Mkoa wa Geita yaliyoandaliwa na Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Kanda ya Ziwa na kufanyika katika Ukumbi wa Hamashauri Geita.
“Najua mmejifunza mengi na mmepata uelewa wa kutosha ili mkienda kwenye shughuli zenu za uchimbaji mkatekeleze kwa vitendo elimu hii mliyoipata ili kuweza kulinda afya za wananchi na mazingira. Tukigundua umepata elimu hii na hautekelezi kwa vitendo elimu uliyoipata basi tutakuchukulia hatua kwa Sheria tulizonazo.
Mnatakiwa kutambua pamoja na kupata fedha kutokana na uchimbaji wa madini ni muhimu kulinda afya za wananchi kutokna na matumizi yasiyo salama ya kemikali ambazo nyie wataalam mnatakiwa kuzisimamia.”
Amewataka kuwa mabalozi kwa wachimbaji ambazo hawajaweza kuhudhuria mafunzo ili kusaidia kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na kemikali zisipotumika vizuri katika shughuli zao.
“Msifunge mdomo mnapotoka hapa kwenda kwenye maeneo yenu ya uchimbaji bali muwe mabalozi kwa kupeleka habari njema ya matumizi salama ya kemikali kwa wenzenu. Elimu mliyoipata mkaitumie kupunguza na kuondoa mapungufu yaliyopo kwenye maeneo ya kazi na hivyo kulinda afya zenu, jamii inayowazunguka na mazingira na ukipata changamoto katika katika matumizi ya kemikali msisite kuwasiliana na wahusika ili kupata msaada.
Mafunzo haya hayataishia kwa kundi la wachenjuaji tu bali yatatolew pia kwa maafisa wa Serikali wanaosimamia maeneo ya uchenjuaji, wamiliki wa maeneo ya uchenjuaji na migodi na baada ya hapo itakuwa imesaidia sana jamii katika kujilinda dhidi ya kemikali na kulinda mazingira” alimaliza.
Akiongea kabla ya mgeni rasmi kufunga mafunzo hayo, Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice Mafumiko, alisema Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali itaendelea kutoa mafunzo kwa wachimbaji wa madini na kufungua ofisi katika Mkoa wa Geita ili kusogeza huduma karibu na wananchi.
“Washiriki wa mafunzo wametupa hamasa kubwa ya kutoa mafunzo ya namna hii mara kwa mara kwa lengo la kusaidia kuongeza uelewa wa matumizi salama ya kemikali katika shughuli za uchenjuaji. Pamoja na utoaji wa mafunzo Mamlaka ina mpango wa kuanzisha ofisi ndogo ya hapa Geita ili kusogeza huduma karibu na wananchi na jamii ya wachimbaji wa dhahabu.”
Jumla ya washiriki 78 walifanikiwa kukabidhiwa vyeti na Mkuu wa Wilaya baada ya kukamilisha mafunzo hayo.
Mkuu wa Wilaya ya Geita, Josephat Maganga (aliyesimama), akiongea wakati wa kufunga mafunzo ya matumizi salama ya kemikali kwa kwa wachimbaji na wachenjuaji wa madini ya dhahabu katika Mkoa wa Geita yaliyoandaliwa na Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Kanda ya Ziwa na kufanyika katika Ukumbi wa Halmashauri ya Mji wa Geita.
Wengine katika picha ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Profesa Esther Hellen Jason (wa pili kushoto), Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice Mafumiko (wa pili kulia), Meneja wa Maabara ya Kanda ya Ziwa, Bonaventura Masambu (kulia) na Katibu Mkuu wa Chama cha Wachimbaji Wadogo Geita, Golden Hainga (kushoto).
Mkuu wa Wilaya ya Geita, Josephat Maganga (aliyesimama), akiongea wakati wa kufunga mafunzo ya matumizi salama ya kemikali kwa kwa wachimbaji na wachenjuaji wa madini ya dhahabu katika Mkoa wa Geita yaliyoandaliwa na Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Kanda ya Ziwa na kufanyika katika Ukumbi wa Halmashauri ya Mji wa Geita.
Mkuu wa Wilaya ya Geita, Josephat Maganga, akimkabidhi cheti cha kuhitimu mafunzo ya matumizi salama ya kemikali Katibu Mkuu wa Chama cha Wachimbaji Wadogo Geita, Golden Haonga (kulia) baada ya kumaliza mafunzo hayo leo.