Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma Dkt. Laurean Ndumbaro mara baada ya watumishi wa ofisi yake kukamilisha zoezi la upandaji wa miti katika mji wa serikali Ihumwa, eneo ambalo Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora inajengwa ili kutoa huduma kwa umma. Dkt. Ndumbaro amesema kuwa, zoezi la upandaji wa miti katika eneo hilo ni endelevu na kuongeza kuwa, Ofisi yake itahakikisha miti hiyo inatunzwa kwa kuimwagilia maji ili hatimaye kuwe na mandhari ya kijani pindi ofisi yake itakapokamilisha ujenzi wa jengo kubwa.
Naye, mmoja wa watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Menyeaichi Koka ameongeza kuwa, watumishi wa Ofisi ya Rais – Utumishi wameitikia wito wa Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan wa kupanda miti ili kulifanya jiji la Dodoma kuwa kijani na kuishukuru menejimenti ya ofisi kwa kusimamia vema zoezi hilo ambalo kila mtumishi amelifanya kwa hiyari na kwa moyo mkunjufu.
Bi. Koka ahaidi kuwa, atahakikisha mti alioupanda anauhudumia vizuri kwa kuumwagilia maji ya kutosha ili uweze kustawi vizuri na kuwa ni miongoni mwa miti iliyopandwa na kufanikiwa kukua vizuri na hatimaye kuchangia jiji la Dodoma kuwa kijani.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan alizindua kampeni za kulifanya jiji la Dodoma kuwa kijani Julai 21, 2017 kwa kuongoza zoezi la upandaji wa miti ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono kwa vitendo uamuzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli wa kuhamishia Makamo Makuu ya Nchi kutoka Dar es Salaam kuja jijini Dodoma.
from MICHUZI BLOG http://bit.ly/2Vh3IqP
via