Amani na usalama vimetajwa kuwa msingi wa mafanikio ya Mwananchi mmoja mmoja na Nchi nzima kwa ujumla. Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule, ameyasema hayo jana jijini Dododma wakati wa kilele cha maadhimisho ya sherehe za miaka 63 ya uhuru wa Tanzania Bara zilizofanyika Kimkoa katika Kata ya Makutupora, Jijini Dodoma.
Mhe. Senyamule aliyekua Mgeni rasmi katika hafla hiyo, amesema Tanzania inajivunia amani na usalama kutoka kwa Waasisi wa Uhuru, na ndio sababu ya maendeleo makubwa tunayoyaona leo hii hasa kwa Mkoa wa Dodoma.
“Tumeshuhudia muundo wa Nchi yetu ulivyo na ushirikishwaji mkubwa wa Wananchi. Mkoa wa Dodoma tunatekeleza kwa vitendo na ndio sababu ya kupata maendeleo haya makubwa. Amani na usalama wa Nchi, ni msingi wa mafanikio, tuvitunze kwa kufanya mambo kwa utaratibu” Mhe. Senyamule
Kadhalika, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mhe. Jabir Shekimweri, amesema “Uhuru wa Nchi yetu unaendelezwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kusimamia vizuri vyombo vya Ulinzi na Usalama, hivyo tunajivunia kuwa na Viongozi madhubuti kwenye awamu zote sita za Uongozi wa Serikali Kuu”.
Sherehe hizo zilitanguliwa na zoezi la upandaji miti katika eneo la Jeshi la JKT Makutupora Kikosi 834, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma aliongoza zoezi hilo kwa kufanikisha kupandwa kwa miti 800 katika eneo hilo.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Prof. Dos Santos Silayo, amesema;
“Tumeshiriki kupanda miti tangu 2017 tulipozindua kampeni ya ‘Dodoma ya Kijani’ katika eneo la Mzakwe ambapo TFS na Jiji la Dodoma tuliingia mkataba wa kuifanya Dodoma ya Kijani, na kuanzia hapo huwa tunatoa miche bure kwa ajili ya kupanda kwenye maeneo yaliyochaguliwa” Prof. Silayo
Hata hivyo, miongoni mwa wadau walioshiriki katika Maadhimisho hayo ndani ya Mkoa wa Dodoma ni mwendesha baiskeli anayejulikana kwa jina la Mwl. Wenseslaus
Justine Lugaya ambaye alianzia safari yake Mkoani Kigoma kwa lengo la kuenzi maadhimisho hayo ambapo alifanikiwa kufika Jijini Dodoma usiku wa kuamkia Desemba 09, 2024.