Siku chache baada ya kutwaa Taji la Miss Tanzania 2014, Sitti Abbas
Zuberi Mtemvu ameibua mshangao wa aina yake kutokana na utata wa umri
wake, Ijumaa limesheheni data.
Utata huo uliibuka saa chache mara baada ya shindano hilo kufanyika
Oktoba 10, mwaka huu kwenye Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar ambapo
wadau mbalimbali walianza kuhoji.
UTATA WENYEWE HUU HAPA
Mara baada ya mrembo
kutangazwa mshindi, habari za chini kwa chini zilidai kwamba Sitti
alijinasibu kuwa ana umri wa miaka 18 na elimu ya (digrii mbili)
(masters), mambo ambayo yaliwashtua wengi na kuanza kuhoji uhalali wa
umri huo ukilinganisha na kiwango chake cha elimu.
“Mh! Haiwezekani,
kama ana miaka kumi na nane atakuwa alianza darasa la kwanza akiwa na
miaka miwili?” Alihoji mdau mmoja ambaye hakupenda jina lake lichorwe
gazetini.
ELIMU YA BONGO IKOJE?
Kwa mfumo wa elimu nchini
ulivyo, mtoto huanza darasa la kwanza akiwa na kati ya miaka mitano hadi
saba, jambo ambalo haliingii akilini kwa Sitti kwani hesabu zinakataa
hata kwa mtu asiyesomea mahesabu.
Ukiachilia mbali shule ya awali (nursery) ambayo huchukua kati ya
miaka miwili hadi mitatu, ukihesabu miaka saba ya elimu ya msingi
(primary), miaka minne ya sekondari (ordinary level), miaka miwili ya
kidato cha tano na sita (advanced level) na miaka mitatu ya shahada
kwanza (bachelor degree), jumla ni miaka 16.
Pia kuna madai kwamba ametumia mwaka mmoja kusomea shahada ya pili
(masters) huku kukiwa na muda ambao kwa kawaida huwa unapotea baada ya
kumaliza kidato cha nne kwenda cha tano na baada ya kumaliza kidato cha
sita kwenda chuo kikuu.
Kwa mantiki hiyo, kama kweli Sitti ana umri wa miaka 18, basi atakuwa
alianza darasa la kwanza akiwa na miaka miwili, jambo ambalo ni msamiati
mpya kwa jamii ya Kibongo.
BABA MZAZI ANASEMAJE?
Ili kuondoa utata na tafrani inayoendelea
kwenye mitandao ya kijamii hadi kufikia hatua ya watu kutukanana, gazeti
hili lilimtafuta baba mzazi wa Sitti ambaye ni Mbunge wa Temeke, Dar
kwa leseni ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Mhe. Abbas Zuberi Mtemvu
alipopatikana alifunguka:
“Umri wake ni kama alivyosema mwenyewe siku ile (miaka 18), kama
mnataka kujiridhisha nendeni hata huko Miss Tanzania mtaoneshwa passport
(hati ya kusafiria) yake…,” alisema mzazi huyo huku akiomba aachwe
kwanza ashughulikie wananchi wa jimboni kwake.
TUMUAMINI MZAZI?
Hata kama tukiamini maelezo ya
mzazi, maana yake ni kwamba mrembo huyo alianza darasa la kwanza akiwa
na miaka miwili, jambo ambalo linazidi kuongeza utata katika sakata
hilo.
Alipobanwa zaidi kuhusu taarifa zinazosema kuwa mwanaye amehitimu
masters, mzazi huyo alikanusha na kudai kwamba mwanaye amehitimu
bachelor degree (shahada).
“Kuhusu masters mnakosea, mwanangu hana
masters, ana bachelor, nilimshauri achukue masters lakini akaomba
nimuache ashiriki kwanza mashindano ya u-miss ndiyo aje aendelee
baadaye,” alisema mheshimiwa huyo.
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari, suala la warembo kudanganya
umri limekuwa ni sugu hivyo kuleta tafsiri ya aibu kwa muandaaji wa
mshindano hayo, Hashim Lundenga akidaiwa kupigwa changa la macho pindi
anapowapokea katika mchakato wa awali.
“Hii ni aibu nyingine kwa Lundenga kwani haiwezekani mtu akaingia
akasema ana miaka kumi na nane halafu awe na elimu kama hiyo,
anashindwaje kulibaini hilo mapema?” Alihoji mdau mkubwa wa urembo
nchini akikumbushia kisa cha Wema Isaac Sepetu, Miss Tanzania 2006/07
ambaye naye alidanganya umri akasema ana miaka 18 wakati alikuwa na kumi
na saba.
MSIKIE LUNDENGA SASA
Alipotafutwa Lundenga ili kuzungumzia suala hilo, alijibu kwa kifupi na kukata simu:
“I can’t answer that question (Siwezi kujibu swali hilo)…siwezi.”
SITTI ANASTAHILI KUWA NA UMRI GANI?
Ukiachilia
mbali muonekano, baadhi ya watu waliozungumza na gazeti hili walisema
kuwa ukifuata utaratibu wa mfumo wa elimu Bongo, Sitti alipaswa angalau
awe na umri wa miaka 23, hata kama madai ya kurushwa madarasa ni sahihi.
Yaani angeanza darasa la kwanza akiwa na miaka saba, angesoma shule
ya msingi kwa miaka saba, sekondari miaka minne, kidato cha tano na sita
miaka miwili na chuo miaka mitatu, jumla angekuwa na umri wa miaka 23
kwa sasa ambayo ni pungufu ya miaka 25 iliyotajwa kwenye wasifu wake
mtandaoni huko nchini Marekani.
SITTI AMEFIKAJE HAPA?
Data zinaonesha kwamba,
baada ya kumaliza kidato cha sita, Sitti alihamia jijini Dalas kwenye
Jimbo la Texas, Marekani ambapo mbali na kusomea elimu ya chuo kikuu
nchini humo, amewahi kuigiza filamu inayojulikana kwa jina la Lost In
Abroad.
CHANZO, GAZETI LA IJUMAA