Mchezaji wa Yanga, Haruna Niyonzima.
Na Wilbert Molandi
WAPO sokoni!
Hivi ndivyo utakavyoweza kutamka baada ya wachezaji watano wa Klabu ya
Yanga kubakiza miezi sita au chini ya hapo kwenye mikataba yao na timu
hiyo.
Kila timu hivi sasa inaangalia nafasi ipi yenye upungufu inayohitaji
kuboresha kwa kusajili wachezaji wenye uwezo kwenye usajili wa dirisha
dogo linalofunguliwa Novemba 15 na kufungwa Desemba 15.
Wachezaji hao watano ruksa kutua kuichezea Simba kwenye mzunguko wa
pili wa ligi kuu ni Mrwanda, Haruna Niyonzima, Mbuyu Twite, Mrisho
Ngassa, Hussein Javu na Mganda, Hamis Kiiza.
Kwa mujibu wa kanuni za Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa),
wachezaji hao wanaruhusiwa kufanya mazungumzo na klabu nyingine kwa
ajili ya kwenda kuichezea kwenye msimu ujao endapo tu watakuwa na
mkataba wa miezi sita au chini ya hapo.
Kwa upande wa Twite, yeye anaweza asiwe kwenye kundi hili kwa kuwa
alisaini mkataba wa mwaka mmoja ambapo kwa sasa ana miezi saba na
ikitokea timu yoyote ikitaka kufanya naye mazungumzo kuanzia Januari,
ruksa.
Wachezaji hao wanne wengine walisaini mikataba ya kuichezea timu hiyo
msimu uliopita, hivyo hadi kufikia Januari, mwaka huu watabakiza miezi
sita itakayowaruhusa kufanya mazungumzo na klabu nyingine
itakayowahitaji.
Alipotafutwa Niyonzima kuzungumzia hilo, alisema: “Nilisaini mkataba
wa miaka miwili msimu uliopita wa ligi kuu, unaotarajiwa kumalizika
msimu huu, hivyo hadi kufikia kipindi cha usajili, nitakuwa nimebakiza
miezi sita.
“Kwa mujibu wa kanuni za Fifa, nitakuwa ninaruhusiwa kufanya
mazungumzo na klabu itakayonihitaji, lakini nisingependa kulizungumzia
hilo kwa hivi sasa kutokana na hali niliyokuwa nayo kwenye timu.”