ILI kukuza kiwango cha ufaulu kwa baadhi ya Halmashauri hapa nchini, Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeandaa mafunzo maalum ya kwa walimu takribani 800 kutoka halmashauri 20.
Mafunzo hayo yanaratibiwa na wizara kupitia Mradi wa uwezeshaji wa elimu (TESP) kwa kushirikiana na ubalozi wa Canada ambapo kwenye hizo halmashauri 20 Shule za Msingi ni nane wakati za Sekondari zikiwa 12.
Akizungumzia mafunzo hayo mmoja wa wawezeshaji kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Dk Alfred Hugo amesema mafunzo hayo yaliyoanza Desemba 10 yatamalizika Desemba 23 na lengo likiwa ni kuwajengea walimu uwezo wa kutambua zana za kufundishia kulingana na mazingira.
” Tunaendesha mafunzo haya kwa walimu wa somo la hisabati kwa Shule za msingi na kwa Sekondari tumezingatia yale masomo ya Sayansi.
Mfano kuna changamoto kubwa ya ufundishaji kwa walimu hasa kwenye masomo ya Sayansi kwa kutokua na vifaa vya kufundishia lakini kupitia mafunzo haya wamejifunza mbinu mbalimbali za kuendana na mazingira waliyopo,” Amesema Dk Hugo.
Amesema kupitia mafunzo hayo walimu wanafundishwa jinsi ya kuwa wabunifu kwenye ufundishaji ili kuwafanya wanafunzi kufurahia masomo na kutoona ugumu wowote hasa kwenye masomo ya Sayansi na Hisabati.
Kwa upande wake mmoja wa walimu walioshiriki mafunzo hayo kutoka Shule ya Msingi Banguma, Bi Nuru Mwendalile ameishukuru Serikali na ubalozi wa Canada kwa kuendesha mafunzo hayo ambayo anaamini yatakua msaada kwao pindi watakaporudi kufundisha.
” Tunaishukuru sana Serikali kwa kutuletea hii fursa. Ni kweli Wilaya yetu ina changamoto za ufaulu lakini tunaamini baada ya kupata mafunzo haya tutayatumia kuboresha kiwango chetu cha ufaulu kwa Shule zetu.
Tumejifunza kubadilika kutokana na mazingira tuliyopo, tumegundua pia hata kama tuna changamoto ya vifaa vya ufundishaji tunaweza kutumia majengo ya madarasa na vitu vingine vya asili kwenye mifano yetu tunapokua tunafundisha,” Amesema Mwalimu Nuru.
from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2tHBfkN
via



