Serikali
kupitia Wizara ya Madini imeanza mazungumzo na Kampuni ya TAQA-DALBIT kwa
ajili ya utekelezaji wa mradi wa upatikanaji wa nishati ya umeme migodini na
maeneo yenye wachimbaji wadogo ili kuchochea shughuli za uchimbaji madini
nchini Tanzania.
Mazungumzo hayo yamefanyika jana Jijini Dodoma na kuongozwa na Waziri wa Madini Mhe. Anthony
Mavunde na Naibu Waziri Madini Mh.
Dkt. Steven Kiruswa pamoja na Menejimenti ya Uongozi wa Kampuni ya TAQA-DALBIT
ikiongozwa na Meneja Mkuu Ndg .Amr Aboushad na Mkurugenzi wa maendeleo
ya Biashara Ndg. Raphael Banzi Akiwasilisha maelezo ya awali,*Ndg. Amr
Aboushad* amesema kwamba Kampuni yao ipo tayari kuja na mpango wa uzalishaji wa
umeme kupitia gesi kwa kufunga mtambo katika migodi na maeneo ya wachimbaji
ambayo itasaidia kupunguza gharama za uzalishaji kwa zaidi ya nusu ya gharama
inayotumika hivi sasa kupitia matumizi ya mafuta ya dizeli na petroli na awamu
ya pili itahusisha uzalishaji wa umeme kupitia mfumo wa umeme jua ambapo
Kampuni itafunga mtambo mkubwa kwa gharama yao na kuwaunganisha wachimbaji
wadogo kwa malipo ya mwezi ya matumizi ya nishati hiyo.
Akizungumza
katika mkutano huo,Waziri wa Madini Mhe. Anthony
Mavunde ameishukuru Kampuni ya TAQA-DALBIT
kwa utayari wa kutatua changamoto ya upatikanaji wa nishati ya umeme migodini
na kuagiza uongozi wa Wizara kuitisha mkutano wa haraka na wadau wote wakiwemo
wachimbaji wadogo na wakubwa ili kupata fursa ya kujadiliana namna bora ya
utekelezaji wa mpango huu. Utekelezaji wa mpango huu utasaidia sana kuchochea
shughuli za uchimbaji nchini Tanzania na hivyo kuongeza uzalishaji wa madini.