Moureen Rogath, Michuzi TV, Buhigwe.
Katika kuhakikisha ufaulu wa wanafunzi wa shule za msingi ni unakua ,wazazi na walimu wameweza kubuni mikakati na miradi mbalimbali kwa lengo la wanafunzi kusoma katika mazingira rafiki.
Akizungumza leo mwalimu mkuu wa shule ya msingi Muyovozi, iliyopo kata ya Biharu wilayani hapa, Alfed Japhet alisema shule zimekuwa na changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa zikijirudia, na kwamba waliazimia kupunguza au kumaliza kabisa.
Alisema walianza kwa kufuga mizinga ya nyuki 10 ambayo wakivuna fedha itaweza kuwasaidia katika mahitaji mbalimbali ya shuleni hapo na si kutegemea fedha kutoka serikali kuu. Mwenyekiti wa shule hiyo Mark Matini, alisema walipokea fedha kiasi cha Sh 1.5 milioni kutoka kwa Mpango wa Kuinua Elimu ya Msingi(Equip), kwa awamu ya kwanza na Sh.550,000 kwa awamu ya pili.
“Fedha hizi zikipatikana zitatusaidia kununua mahitaji muhimu kwa shule na wanafunzi mfano, taulo za kike, kuwaboreshea miundombinu kwani kama wananfunzi atasoma kwa shida hata ufaulu wake utakuwa mbaya,”alisema mwenyekiti wa shule huyo.
Alisema serikali kwa kushirikiana na Equip iliweza kuleta mpango wa maendeleo ya kadi ya shule ambayo itamuwezesha mzazi kusoma taarifa mbalimbali na maendeleo ya shule ikiwemo mapato na matumizi hali iliyopunguza malalamiko kwao.
“Kabla ya kuwepo kwa kadi ya maendeleo ya shule kulikuwa na malalamiko kutoka kwa wazazi na walezi lakini baada ya kuweka taarifa zote za shule kwenye ubao huo ushirikiano umekuwa mkubwa.
Mzazi na mkazi wa eneo hilo Nostord Legero, alisema baada ya shule hiyo kuja na utaratibu wa kadi ya maendeleo ya shule imewasaidia wao kujua taarifa mbalimbali na kwamba wako tayari kutoa ushirikiano kwa uongozi bila kuwa na mashaka.
Afisa elimu na mratibu wa Equip wilaya ya Buhigwe Noel Kasaya, alisema shule 88 za wilaya zina kadi ya maendeleo ambayo lenye lengo la kuwapa taarifa za shule wazazi na walezi kupunguza maswali na malalamiko yanayoweza kujitokeza.
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Muyovozi, iliyopo kata ya Biharu wilayani Buhigwe mkoani Kigoma, Alfred Japhet,akionyesha kadi ya maendeleo ya shule iliyochorwa kwa lengo la wazazi na walezi kupata taarifa za shule na kupunguza malalamiko.
Mradi wa ufugaji wa nyuki katika shule ya msingi Muyovozi ,uliobuniwa na waalimu wa shule hiyo pamoja na wazazi kwa lengo la kujipatia kipato na kutatua changamoto zinazowakabili shuleni hapo ikiwemo ununuzi wa taulo za kike kwa wanafunzi na kuboresha miundombinu kwa msaada wa fedha za Equip ikiwa ni mizinga 40 ya nyuki.
from MICHUZI BLOG https://ift.tt/2YFOWeG
via


