Mwandishi Wetu
WAMESHTUKA! Wakati siku zikizidi kuyoyoma kuelekea uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani utakaofanyika Oktoba 25, mwaka huu kote nchini, hamahama ya mastaa kutoka chama kimoja kwenda kingine ina maana kuna jambo wameshtukia? Risasi Mchanganyiko linakupa zaidi.
Zikiwa zimebaki siku 39 kabla ya Watanzania kuelekea vituoni wakiwa na ‘vichinjio’ vyao kwa ajili ya kumchagua kiongozi anayewafaa, gazeti hili linaweza kuthibitisha pasipo shaka kuwa angalau wasanii kadhaa wa muziki na filamu wameasi kambi zao za awali na sasa wapo upande wa pili.
TUJIUNGE NA CHANZO
Kwa mujibu wa chanzo makini, baadhi ya wasanii wa filamu ambao awali walikuwa kwenye Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Vincent Kigosi ‘Ray’ na Aunt Ezekiel wanadaiwa kuzengewa ili nao warejee Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Duru za kisiasa kwenye ulimwengu wa mastaa Bongo zinasema harakati za kuwanasa wawili hao zilianzia katika Viwanja vya Leaders Club, Kinondoni jijini Dar es Salaam, zikitajwa kuratibiwa na mwigizaji mkongwe, Single Mtambalike ‘Richie’.
Richie anadaiwa kuandamana na kada mmoja wa CCM ambaye ndiye hasa aliyefanya mazungumzo na Ray, aliyeingia katika viwanja hivyo akiwa katika gari jipya ambalo namba zake za usajili zilikuwa hazionekani.
Wakati hali ikiwa hivyo kwa Ray, chanzo kingine kinadai kuwepo kwa vikao mfululizo kati ya mawakala wa CCM na muigizaji mwingine nyota, Aunt Ezekiel ili kumshawishi kuachana na Ukawa ili aelekeze nguvu zake chama tawala.
Ray hakuweza kupokea simu yake ya mkononi baada ya kutafutwa ili kutoa ufafanuzi wa suala hilo, lakini Richie alipatikana na kulizungumzia suala hilo kwa kina.
“Ni kweli nilikuwa na Ray pale Leaders kwa muda huo unaosema, ni kweli pia kuwa mimi ni CCM kindakindaki, lakini kusema kuwa nilikuwa mshenga wa kumleta huku siyo kweli. Ray ni mwanangu, kwa hiyo kuongea naye siyo jambo baya, hata kama yeye ni Ukawa.
“Unajua unaposikia ushabiki wa Simba na Yanga siyo uadui, watu mnakaa pamoja na kuongea, kama mtu anaweza kumshawishi mwenzake kuhama ni jambo la kawaida,” alisema mwigizaji huyo nyota.
TETESI MPYA
Wakati hayo yakijiri, habari kutoka chini ya kapeti zinasema kuwa mwigizaji mwingine, Shamsa Ford naye anawindwa kutoka kundi la wasanii mashabiki wa Ukawa, ambao wanafanya kampeni ili kumpa ushindi mgombea wao, Edward Lowassa.
“Sijawahi kushawishiwa kutoka Ukawa, siwezi kutoka Ukawa, nitaendelea kuwa Ukawa kwa muda wangu wote,” alisema nyota huyo kuonesha kwamba naye ameshtuka!
WALIOIHAMA KAMBI KABLA
Wasanii wengine walio katika orodha ya kuhama kambi wanasemwa kuwa ni pamoja na mkongwe wa Bongo Fleva, Juma Kassim maarufu kama Nature, ambaye anatajwa kuachana na Ukawa ili arejee CCM.
Lakini katika mahojiano na gazeti hili wiki iliyopita, Nature alisema ni kweli hivi sasa atafanya shoo katika kampeni za CCM, lakini akisisitiza kuwa anafanya hivyo kwa kuwa yeye ni msanii na hiyo ni kazi yake.
Katika orodha hiyo pia yupo msanii wa filamu, Chuchu Hans ambaye awali alikuwa Chadema na Ukawa na kuvaa sare zao siku ya ufunguzi wa kampeni lakini siku chache baadaye aliamua kurudi CCM huku listi ikiongezwa na msanii wa vichekesho, Kitale.
HAWA WAMEJIPAMBANUA
Pia wapo wasanii ambao kwa muda wote wamejulikana kuwepo kambi moja wakiwa ni pamoja na Steven Mengere ‘Steve Nyerere’ (anadaiwa kuposti mitandaoni maneno ya kuwakaribisha Ray na Aunt kujiunga na CCM), Wema Sepetu, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, Ali Kiba, Sabrina Rupia ‘Cathy’, Salome Urassa ‘Thea’, Davina ambaye jina lake halisi ni Halima Yahya na Rutta Bushoke ambao wanafahamika kuwa ni CCM damu.
Wasanii ambao wamejipambanua kuwepo Ukawa pamoja na wengine ni Jacqueline Wolper, Emmanuel Elibariki ‘Nay wa Mitego’, Husna Idd ‘Sajenti’, Haji Adam ‘Baba Haji’ na Kala Jeremiah, Jimmy Mafufu, Bob Junior, AT na Soggy Doggy.