Boti inayosafirishwa kutoka Mtwara kuelekea Mwanza kupitia mikoa tisa kwa ajili ya uokozi ziwa Victoria ikiwa imeanza safari yake.
Na Regina Ndumbaro-Mtwara
Boti kubwa ya uokozi kwa ajili ya Ziwa Victoria imeanza safari yake ya kusafirishwa kutoka mkoani Mtwara kuelekea Mwanza, ikiwa ni juhudi za serikali kuimarisha shughuli za uokoaji kwenye ziwa hilo.
Boti hiyo, yenye urefu wa mita 29, upana wa mita 5.6 na kimo cha mita 7.4, inatarajiwa kuwa msaada mkubwa katika shughuli za dharura na usalama wa abiria na mali katika ziwa hilo maarufu.
Usafirishaji wa boti hiyo unafanywa kwa njia ya barabara na kampuni ya Raphael Logistics, ambapo inatarajiwa kupita katika mikoa tisa ya Tanzania bara.
Mikoa hiyo ni Mtwara, Ruvuma, Njombe, Iringa, Morogoro, Dodoma, Tabora, Shinyanga na hatimaye Mwanza.
Safari hiyo itachukua muda wa wiki tatu hadi nne, sawa na takribani mwezi mmoja, kutokana na ukubwa na uzito wa boti hiyo ambayo inakadiriwa kuwa na tani 26.
Kutokana na ukubwa wake, mamlaka za usafirishaji na usalama barabarani zimetahadharisha watumiaji wa barabara katika mikoa husika kuwa waangalifu na kuchukua tahadhari zote muhimu wakati msafara huo utakapokuwa ukipita.
boti hiyo inasafirishwa kwa uangalizi maalum ili kuhakikisha inafika salama katika makazi yake mapya jijini Mwanza.
Boti hiyo inatarajiwa kuongeza uwezo wa haraka wa kutoa msaada kwenye Ziwa Victoria, ambalo limekuwa likikumbwa na ajali za mara kwa mara zinazohitaji uwepo wa vifaa vya kisasa vya uokoaji.
Mradi huu ni sehemu ya maboresho ya usafiri wa majini na juhudi za serikali katika kulinda maisha ya wananchi wanaotegemea ziwa hilo kwa shughuli zao za kila siku