Bunge la Tanzania limepinga vikali baadhi ya maazimio yaliyotolewa na Bunge la Ulaya kuhusu masuala ya kisiasa na kijamii ya ndani ya nchi, likilenga hasa hoja ya kutambua mapenzi ya jinsia moja. Wakati huo huo, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetoa msimamo wake rasmi ikisisitiza kuwa hatua zote za kisheria dhidi ya viongozi au raia zinafuata misingi ya utawala wa sheria.
Wabunge wakizungumza leo mjini Dodoma, wameonyesha kutoridhishwa na azimio la pili la Bunge la Ulaya linalohimiza Tanzania kutambua haki za wapenzi wa jinsia moja, wakilitaja kuwa ni dharau kwa taifa na kinyume na misingi ya kijamii na kiimani ya Watanzania.
Mbunge wa Biharamulo Magharibi, Ezra John Chiwelesa alisema:
“Yalitolewa maazimio 6 kwa ajili ya Serikali ya Tanzania, na moja ya azimio ni kuhusu Tundu Lissu, hiyo sina shida nayo kesi iko Mahakamani, lakini lipo azimio namba mbili la kutambua haki ya mapenzi ya jinsia moja.”
Aliongeza:
“Kwangu mimi nimeona ni dharau kwa nchi yetu, ni dharau kwa Mungu, hatujafikia hatua ya kudharaulika kiasi hiki tuandikiwe na watu sasa kwamba tutambue haki za mapenzi ya jinsia moja. Kwa niaba ya Watanzania tunaowawakilisha kupitia ndani ya Bunge hili, masuala haya ya laana katika nchi hii hatuyahitaji,” alisema.
Mbunge wa Tarime Vijijini, Mwita Waitara, naye alieleza:
“Nilipoona walichoandika watu wa Ulaya, kama hoja yao ni kwamba wasilete maji, basi tutakunywa hata maji ya kisima,” alisema Waitara, akishangiliwa na wabunge wenzake. Habari ya mapenzi ya jinsia moja waendelee wao, sisi tusonge mbele. Naamini serikali ya Chama cha Mapinduzi na sisi wabunge makini hatuwezi kuunga mkono upuuzi wa namna hiyo.”
Maazimio yaliyojadiliwa ni yapi?
Wameitaka Serikali ya Tanzania kumwachilia mara moja Lissu na bila masharti yoyote, ili kuhakikisha usalama wake na haki yake ya kusikilizwa kwa haki na uwakilishi wa kisheria.
Wabunge hao wanazitaka mamlaka za Tanzania kukomesha ukandamizaji unaoendelea, ukamataji hovyo, unyanyasaji, mashambulizi na unyanyasaji dhidi ya wanachama wa upinzani, watetezi wa haki za binadamu, watu wa kiasili, wanaharakati wa LGBTIQ+, waandishi wa habari na mashirika ya kiraia, na kuchunguza kwa uhuru dhuluma za polisi na kupotea kwa watu, kudumisha utawala, sheria, vyombo vya habari, uhuru wa kujieleza, uhuru wa vyombo vya habari na mahakama.
Sheria za uhalifu wa mtandaoni na vyombo vya habari za Tanzania kwa zizingatie sheria za kimataifa za haki za binadamu, kuheshimu haki za vyama vya siasa na kuhakikisha uchaguzi huru na wa haki.
Wito kwa mamlaka za Tanzania kurejesha ushiriki kamili wa Chadema katika uchaguzi wa Oktoba 2025 na kushirikiana na vyama vyote vya siasa katika mazungumzo ya uwazi na jumuishi kuhusu mageuzi ya uchaguzi, kwa kushauriana na mashirika ya kiraia na wadau wengine.
Wito kwa EU na nchi wanachama wake kuwasiliana kwa kina na mamlaka za Tanzania kuhusu kesi ya Lissu na kufuatilia kwa karibu kesi; inawataka kuzingatia hatua zinazofaa ikiwa hali ya haki za binadamu itaendelea kuzorota.
Wanaitaka Tanzania kufuta hukumu ya kifo na kubadilisha hukumu zote za kifo.
Wanasisitiza haja ya EU kuhakikisha kwamba ushirikiano wake wa kimaendeleo na Tanzania, ikiwa ni pamoja na mpango wa Global Gateway, unaendana na uendelezaji wa haki za binadamu, uhuru wa kujieleza na viwango vya kesi vyenye haki.
Wabunge hao wanamuagiza Rais wake kupeleka azimio hilo kwa Serikali na Bunge la Tanzania pamoja na Umoja wa Afrika.
Azimio hilo linatarajiwa kupigiwa kura na wabunge hao leo Alhamisi tarehe 8.